Saturday, 26 March 2016

Bodaboda Mkoani Mwanza wataka kuanzishwa kwa Umoja wa Kitaifa wa Bodaboda


 Na Renalda Mwarabu

 
Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza Baraka Konisaga (Mtumishi wa Mungu) akuzungumza katika Mkutano Mkuu Muhula wa Kwanza wa mwaka 2016 wa Umoja wa Waendesha Bodaboda Mkoa wa Mwanza uliofanyika Jumamosi Machi 19,2016 katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Pamba Jijini Mwanza. Kushoto kwake ni viongozi wa bodaboda Mkoa wa Mwanza.


Umoja wa waendesha Bodaboda Mkoa wa Mwanza  kwa paamoja wamekubaliana kwa sauti moja kuanzishwa kwa Umoja wa Bodaboda Taifa ili kurahisisha utatuzi wa Changamoto zinazoikabiri sekta ya usafirishaji abiria ya  kwa njia hiyo ya Bodaboda.
Kufuatia mkutano wao Mkuu wa mwaka ambao mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Mkoani Mwanza Baraka Konisaga (pichani) ambae alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.

Katika Mkutano huo, Konisaga ambae alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, alitaka jeshi la polisi kitengo cha usalama barabara kuzidisha juhudi za kutoa elimu ya usalama barabarani ili kupunguza ajali, badala ya kasi iliyopo ya kutoza faini kwa watumiaji wa vyombo vya barabarani.

Mwenyekiti wa bodaboda Mkoa wa Mwanza Makoye  Kayanda amesema "pamoja na Mambo mengine, Wajumbe wa Mkutano huo walikubaliana kwa sauti moja kuanzishwa kwa Umoja wa Bodaboda Taifa ili kurahisisha utatuzi wa Changamoto zinazoikabiri sekta ya usafirishaji abiria ya Bodaboda".

Amesema miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na kuvamiwa, kutekwa, kuuawa na kuuawa kwa waendesha bodaboda huku bodaboda zao zikiibiwa. Kutafuta suluhu ya baadhi ya watu wakiwemo bodaboda kutumia fursa hiyo katika kujihusisha na uhalifu nchini. 
 
Utii wa Sheria bila shuruti pamoja na kujadili namna bodaboda wanavyoweza kushirikiana na taasisi mbalimbali zikiwemo za binafsi na Serikali kwa ajili ya maendeleo ya sekta hiyo.

Mkutano huo ulihudhuriwa na Viongozi wengine wa Bodaboda kutoka Mikoa ya Mara, Tabora, Singida, Shinyanga, Kilimanjaro pamoja na Viongozi wa sekta nyingine ambazo ni wadau wa usafirishaji ambao ni Machinga, Mamalishe, Daladala, Mabasi, RTO, Sumatra pamoja na TRA. Chanzo Mo blog

Nchi za Afrika Mashariki kuunda Jeshi la Pamoja


Na Renalda Mwarabu


Jumuiya ya Afrika Mashariki ,EAC, inakaribia kuunda jeshi la pamoja kwa lengo la kulinda taasisi muhimu za kiuchumi za nchi wanachama.

Hayo yamebainika wakati wa mafunzo ya pamoja mjini Nairobi ya wanajeshi 300 kutoka Kenya, Uganda, Tanzania, Burundi na Rwanda.

Kamanda wa Majeshi ya Kenya Jenerali Samson Mwathethe amesema kikosi hicho cha pamoja ni muhimu kwa kuzingatia matarajio makubwa ya ustawi wa kiuchumi Uganda na Kenya kutokana na uzalishaji mafuta na gesi asilia Tanzania.

Akizungumza Ijumaa wakati wa mazoezi hayo Jenerali Mwatheteh amesema, “Shirikisho limeanza kupata muundo wake hatua kwa hatua kama ilivyopangwa na nchi zote za EAC ikiwemo Sudan Kusini. Eneo hili lina ukubwa wa mita mraba milioni 2.4 na idadi ya watu milioni 170.

 Nchi zote wanachama zinafungamana na udumishwaji amani na usalama katika eneo.”

Mkuu wa Jeshi la Kenya amesema ugaidi ni tishio kubwa zaidi la usalama katika eneo na hivyo nchi zote zinapaswa kushirikiana. Akizungumza katika hafla hiyo Waziri wa Ulinzi wa Kenya 

Raychelle Omamo amesema mafunzo hayo ya maafisa wa kijeshi ni katika fremu ya ushirikiano wa kiulinzi baina ya nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. 

Aidha amesema vikosi vya usalama vinapaswa kufahami mbinu za makundi ya kigaidi yanayolenga kuvuruga uchumi wa eneo hilo. Chanzo radio Terhan

Thursday, 17 March 2016

Jeshi la Cameroon laangamiza B/Haram 20 nchini Nigeria

Na Renalda Mwarabu
  
Jeshi la  Cameroon limetangaza kuwa limefanikiwa kuangamiza wanachama 20 wa kundi la kigaidi  la Boko Haram katika operesheni iliyofanyika huko kaskazini mwa Nigeria.

Kanali Jacob Kodji, kamanda mwandamizi wa jeshi la Cameroon amesema kuwa, operesheni hiyo ya jana Jumatano ya kuwaangamiza wanamgambo wa Boko Haram ilifanyika katika mji wa Djibrila, yapata kilomita 10 kutoka mpaka wa Cameroon.

 Naye Msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Cameroon, Kanali Didier Badjeck amesema mateka 12 wameokolewa kutoka mikononi mwa magaidi hao sambamba na kupata silaha na magari ya kijeshi yaliyokuwa yameibiwa na matakfiri wa Boko Haram.

 Operesheni ya Jumatano dhidi ya Boko Haram imefanyika siku moja baada ya wanachama wa kundi hilo la kigaidi kuua watu 22 waliokuwa wakisali katika msikiti wa jimbo la Maiduguri, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.

 Hii ni katika hali ambayo, serikali ya Benin imesema kuwa, mwezi ujao nchi hiyo itatuma kikosi cha askari 150 watakaojiunga na kile kinachoundwa na nchi kadhaa ambacho kimekuwa kikikabiliana na wanamgambo wa Boko Haram ambao wamehatarisha usalama katika nchi ya Nigeria na katika mipaka ya nchi nyengine ikiwemo Cameroon.

 Inadaiwa kuwa kuna wanamgambo 8700 wa Boko Haram kwenye eneo hilo. 

Watu zaidi ya 20,000 wameuawa na wengine zaidi ya milioni 2.5 wakilazimika kuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi tangu kundi la Boko Haram lianzishe hujuma zake nchini Nigeria mwaka 2009

Monday, 7 March 2016

Mahakama Singida yawahukumu majangili saba kwenda jela miaka 140 na faini ya Bilioni 1.9

Na Renalda Mwarabu


Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini Singida, imewahukumu majangili saba adhabu ya kutumikia jela ya miaka 140 na kulipa faini ya zaidi ya shilingi 1.9 bilioni baada ya kuwatia hatiani kwa kwa makosa 12  likiemo la kumiliki bunduki ya kijeshi SMG waliyokuwa wanaitumia kuulia Tembo.

Baadhi ya makosa mengine ni kuunda umoja /ushirikiano wa kufanya uhalifu wa  kuuawa  wanyapori wakiwemo Tembo, kufanya biashara haramu ya kuuza nyara za serikali na kumiliki meno ya Tembo bila kwa na kibali.

Washitakiwa hao ambao kesi yao ilipewa namba 5/2015, ni Yusuph Masala Jidavi (39) mkulima kijiji cha Yongo Manda mkoani Katavi, Elias John  Sprian (30) mkazi wa Kijiji cha Ng’ambe mkoani Tabora na Salum Mohammed Ngasa (31) mkazi wa kijiji cha Imalampaka Sasilo wilaya ya Manyoni.

Wengine ni Yona  Stanley @Yohana (26) mkazi wa kijiji cha Mbwasa Sasilo wilaya ya Manyoni, Ramadhani Salum Hatibu (33) mkulima kijiji cha Mgulu wa Ng’ambe wilaya ya Manyoni,Kulwa Saidi Salum (28) mkulima kijiji cha Sikonge mkoani Tabora na Buhoro Salehe Lubaha Yakonie (37)@  Buhoro  mkazi wa Kambi ya Wakimbizi Katumba mkoani Tabora.

Mwendesha mashtaka na mwanasheria wa serikali Pretrida Mutta, alidai mbele ya Hakimu mfawidhi mwandamizi na mahakama hiyo, Joyce Minde, kuwa kati ya Agosti mwaka 2013 na Julai nane mwaka 2014, washitakiwa kwa pamoja walikamatwa wakimiliki vipande 28 vya meno ya Tembo vyenye thamani zaidi ya shilling 34.1 milioni.

Mutta alisema pia washitakiwa hao walikamatwa wakimiliki kinyume na sheria ‘Elephant tufts’ sita zenye thamani ya shilingi 192 milioni, kipande cha ngozi ya Simba chenye thamani ya zaidi ya shilingi 7.8 milioni na ngozi ya kudu ya shilingi 3.5 milioni.

Kabla ya kutolewa kwa hukumu, Mwanasheria wa serikali Mutta, aliiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa washitakiwa, ili iwe fundisho kwao na kuogofya watu wengine wanaotarajia kujihusisha biashara haramu ya kuuza nyara za serikali.

Kwa upande wa washitakiwa ambao wakili wao na kujitegemea Josephat Wawa ambaye hakuwepo Mahakamani, washitakiwa kila mmoja kwa wakati wake, aliiomba mahaka hiyo impe adhabu nafuu kwa madai mbalimbali likiwemola kutegemewa na familia.

Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Minde, alisema kuwa upande wa mashitaka umethibitisha bila kuacha chembe chembe ya shaka kwa hali hiyo washitakiwa wana hatia kama walivyoshitakiwa.
“Kila mshitakiwa atatumikia jela miaka 20 na kulipa faini ya zaidi ya shilingi 274.2 milioni adhabu hizi ni fundisho kwenu na pia kuwaogofya watu wengine wanaotarajia kutenda makosa ya aina hii”,alisema Hakimu Minde.Chanzo Radio Terhan.

Daesh: Tutaishambulia Russia kwa kulipiza kisasi


Na Renalda Mwarabu
 
Kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh limetishia kupitia mkanda wa video kuwa, litafanya shambulio la kigaidi nchini Russia kama ulipizaji kisasi.

Katika mkanda huo uliorushwa jana katika mitandao ya kijamii, kundi hilo la kigaidi limetishia kushambulia kila mahala palipo na maslahi ya Russia kwa kile kundi hilo limesema, ni kulipiza kisasi kutokana na kuuawa wanachama wake wengi katika mashambulizi ya anga ya Russia nchini Syria.

 Mwanzoni mwa mkanda huo, Daesh sanjari na kutangaza kuhusika na mripuko ulioua polisi wawili nchini Dagestan, imeonyesha gari ililotumia kutekeleza shambulio hilo na ambalo lilikuwa limesheheni mada za miripuko. 

Aidha kundi hilo ambalo limepata hasara kubwa kufuatia mashambulizi ya ndege za Russia nchini Syria, limeonyesha likimuua mtu mmoja ambaye kwa mujibu wa Daesh, ni afisa wa upelelezi wa nchi hiyo aliyekamatwa na wanachama wa genge hilo ingawa haijabainika ukweli wake.

 Hadi sasa bado serikali ya Moscow haijatoa maelezo yoyote kuhusiana na mkanda huo wa vitisho wa kundi hilo la kigaidi.

Kwa kipindi cha miezi mitano sasa Russia, imekuwa ikiendesha mashambulizi makali dhidi ya wanachama wa kundi la Daesh na Jab'hatu Nusra nchini Syria, mashambulizi yanayotajwa kuwa na mafanikio makubwa. Chanzo Radio Terhan

Saturday, 5 March 2016

UN: Maelfu ya Warundi wamekimbilia nchi jirani

 Na Renalda Mwarabu
    
Kamishna Mkuu wa Wakimbizi wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa maelfu ya Warundi wamekimbilia katika nchi jirani.

Msemaji wa Kamisheni Kuu ya Wakimbizi ya Umoja wa Mataifa, Melissa Fleming amesema kuwa,  tangu Aprili mwaka 2015 hadi sasa wakimbizi laki tano na 946 wa Burundi wamekimbilia katika nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Tanzania, Rwanda, Uganda na Zambia.

Melissa Fleming ameongeza kuwa hadi sasa hakujapatikana maendeleo ya maana katika uwanja wa haki za binadamu na usalama wa ndani nchini Burundi licha ya juhudi zote zilizofanyika na kwamba hali mbaya ya uchumi yumkini ikazidisha idadi ya wakimbizi katika siku za usoni.

Machafuko ya ndani nchini Burundi yalianza baada ya Rais Pierre Nkurunziza kutangaza nia yake ya kuwania tena kiti hicho kwa mara ya tatu mfulilizo. Wapinzani wanasema hatua hiyo ilikiuka katiba ya nchi na makubaliano ya amani ya Arusha yaliyohitimisha vita vya ndani.(Chanzo Radio Terhan)

Ripoti: Israel inawaua kwa makusudi watoto Palestina

         Na Renalda Mwarabu    
        
Harakati ya Kimataifa ya Kuwalinda Watoto imeripoti kuwa wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wanawauwa kwa makusudi watoto wa Kipalestina.
 
Harakati ya Kimataifa ya Kuwalinda Watoto tawi la Palestina leo imeashiria kitendo cha wanajeshi wa Kizayuni cha kuwauwa shahidi watoto 41 wa Kipalestina tangu kuanza Intifadha ya Quds hadi sasa, na kusisitiza kuwa wanajeshi wa utawala huo wanatekeleza siasa za kuwafyatulia risasi kwa makusudi watoto wa Kipalestina kwa lengo la kuwauwa, hatua ambayo ni kinyume na sheria.
 
Harakati hiyo imeashiria kuuliwa shahidi watoto 16 wa Kipalestina waliopigwa risasi na askari wa Israel katika mwaka huu wa 2016 na kuongeza kuwa, utawala huo umefunga mafaili ya mauaji ya watoto hao bila ya kufanya uchunguzi na umepinga pia ombi la familia za wahanga wa mauaji hayo waliotaka maiti za watoto wao zifanyiwe uchunguzi.
 
Tangu kuanza Intifadha ya Palestina hadi sasa, makumi ya watoto wa Kipalestina wameuawa shahidi kwa kupigwa risasi kwa makusidi na wanajeshi wa Israel katika maeneo mbalimbali ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, Quds na Ukanda wa Ghaza. Chanzo Radio Terhan



Friday, 4 March 2016

Museveni asema hatogawana madaraka na wapinzani

Na Renalda Mwarabu
 
Rais Yoweri Museveni wa Uganda amesema hawezi kugawana madaraka na kambi ya upinzani kwani alishinda kihalali kwenye uchaguzi mkuu wa Februari 18.

Akizungumza na kiongozi wa chama cha upinzani cha Farmers Party of Uganda (FPU), Meja Jenerali Benon Biraaro, Rais Museveni amesema anakaribisha pendekezo la kufanya mazungumzo na wapinzani kwa ajili ya kujadili mustakabali wa kisiasa wa taifa lakini hawezi kuunda serikali ya umoja wa kitaifa itakayowashirikisha wanasiasa wa upinzani.

Amesema uchaguzi ulikuwa fursa nzuri kwa wanasiasa kujitafutia vyeo na kama wapinzani walishindwa kuwashawishi wapiga kura, wanapaswa kusubiri hadi uchaguzi ujao na wala si kutumia njia za mkato kuingia serikalini.

Huku hayo yakijiri kuna tetesi kwamba kiongozi wa upinznai, Kizza Besigye ametoweka na hajulikani aliko. Duru za habari zinasema Besigye ambaye alikuwa chini ya kifungo cha nyumbani hayuko tena nyumbani kwake. Polisi ya Uganda imekataa kuthibitisha au kukanusha suala hilo.( Chanzo Radio Terhan)

TAZAMA VIDEO HII INAYOHUSU NIDHAMU .

Mwandaaji ni 
Renalda Mwarabu na Jane Mafupa

Ban na wasiwasi na kuenea misimamo mikali Afrika

Na Renalda Mwarabu

 Katibu mkuu wa umoja wa mataifa Bwana Ban Ki Moon akitoa wasiwasi wake juu kuhusu mashambulizi ya kigaidi barani Afrika.
 
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, ameelezea wasiwasi wake kuhusu mashambulizi ya makundi ya kigaidi huko Burkina Faso, magharibi mwa Afrika na kuitaka dunia isimame kukabiliana na hatari ya kuenea misimamo mikali barani Afrika.

Ban Ki moon amesema hayo huko Ouagadougou, mji mkuu wa Burkina Faso na kuongeza kuwa, nchi za ukanda huo zinapaswa kushrikiana kukabiliana na matatizo mbalimbali kama vile umaskini, ukosefu wa kazi, ubaguzi na kinga ya kutoshitakiwa baadhi ya watu.

Ban alianza ziara yake ya kuzitembelea nchi kadhaa za Afrika siku ya Jumatano kwa kuanzia nchini Burkina Faso ambako alilakiwa na Alpha Barry, Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo.

Jana Alkhamisi alionana na Rais Roch Marc Christian Kaboré wa nchi hiyo, kama ambavyo alitembelea pia kituo kimoja na kuwasaidia chakula watoto wadogo na kituo kimoja cha watoto wenye maradhi ya Ukimwi.

Mbali na Burkina Faso, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amepangiwa kutembelea pia nchi za Mauritania na Algeria.

Ziara ya Ban Ki moon inafanyika katika hali ambayo hivi karibuni kulitokea mashambulio ya kigaidi katika mji mkuu wa Burkina Faso, Ouagadougou na kupelekea kuuawa zaidi ya watu 30. Chanzo Radio Terhan

Thursday, 3 March 2016

Serikali yavipongeza Vyombo vya Habari kwa kuhabarisha jamii vyema

Na Renalda Mwarabu

Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Anastazia Wambura akizungumza na wadau wa Habari akivishukuru vyombo vya habari kwa kuhabarisha watanzania kipindi cha uchaguzi na pia katika siku mia za kwanza za Rais wa awamu ya tano na Mhe.John Pombe Magufuli na kuwapongeza kwa kuonyesha weledi na ukomavu katika uandishi wa Habari.
Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe. Anastazia James Wambura amevipongeza Vyombo vya Habari kwa kuwahabarisha watanzania vyema katika mchakato wote wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 na katika kipindi cha siku mia za kwanza za awamu ya tano ya utawala wa Mheshimiwa Dr. John Joseph Pombe Magufuli.

Naibu Waziri uyo ameyasema hayo alipokuwa akiongea na wadau wa Habari katika tafrija fupi iliyoandaliwa na kampuni ya Mwananchi Communications Limited.

“Hakika mmeonesha uwezo mkubwa, weledi na ukomavu mkubwa wa kisiasa na uzalendo kwa nchi yetu”.Alisema Bi.Wambura.

Mhe.Wambura pia alieleza kuwa Serikali ya awamu ya tano ina dhamira ya dhati kabisa ya kushirikiana na wadau wote vikiwemo Vyombo vya Habari, ambapo pia mchakato wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ambao ulishasomwa kwa mara ya kwanza bungeni bado Serikali inaendelea kupokea maoni ya wadau mbalimbali juu ya namna bora ya kuboresha Muswada huo.

Naibu Waziri uyo alikazia umuhimu wa upashaji habari na kusema ni jambo muhimu sana katika nchi yetu na kwaiyo Wizara ya Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo iko tayari kufanya kazi na wadau wote.

“Kama Serikali hatuwezi kuwakwepa wadau na ndio maana hata utaratibu wetu wa kushughulikia makosa kwenye Vyombo vya Habari umebadilika. Tumekuwa ni walezi zaidi badala ya kuwa viranja. Tunashauriana zaidi kuliko kutoa adhabu. Tunaelimisha zaidi kuliko kusubiliana”

Naibu Waziri uyo pia ameupongeza uongozi mpya wa jukwaa la wahariri na kuhaidi kuwapa ushirikiano wa karibu katika kutatua masuala mbalimbali ya Habari.

Kwa upande wake Mwenyekiti Mtendaji wa Bodi ya Magazeti ya Mwananchi Bw.Francis Nanai ameipongeza serikali kwa kuweka jitihada zaidi katika kuboresha mahusiano mazuri na vyombo vya Habari na pia kwa afrika mashariki Tanzania iko katika nafasi nzuri ukilinganisha na wenzetu katika suala la uhuru wa vyombo vya habari.
(Chanzo Mo bog)